Zikiwa zimepita siku 16 tangu Frateri wa Kanisa Katoliki, Rogassian Massawe (25) anayedaiwa kujinyonga hadi kufa azikwe nyumbani kwao, katika Kijiji cha Umbwe Onana, Wilaya ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, mama yake mzazi, Levina Hugo (58) naye amefariki dunia.
Frateri huyo alizikwa Mei 25, 2024 baada ya kudaiwa kujinyonga kwa kutumia mshipi Mei 20, mwaka huu akiwa kwenye nyumba yao ya malezi ya Magamba iliyopo wilayani Lushoto, mkoani Tanga.
Kabla ya kutekeleza hilo, Frateri Massawe inadaiwa kuwa aliacha ujumbe wa maandishi kwa mama yake mzazi uliosomeka; “mama usilie, nimeshindwa kufikia malengo, najua nimewakwaza wengi."
Siku ya maziko Mei 25, 2024 nyumbani kwao, ndugu wa familia hiyo, Padri Andrea Hugo, aliwaomba waombolezaji kuiombea familia hiyo kwa kuwa mama yake mzazi Frateri huyo aliugua ghafla na kulazwa Hospitali ya KCMC, hivyo hakuweza kushiriki maziko ya mwanaye kwa mshituko alioupata.
Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumatatu Juni 10, 2024, nyumbani alikozaliwa mama huyo eneo la Umbwe Onana, wilayani Moshi, mdogo wa marehemu, Jerome Aloyce amesema wamepata pigo lingine kwenye familia.
Aloyce amesema wapo kwenye wakati mgumu sana kwa sababu wamepoteza watu wawili ndani ya muda mfupi.
"Dada yetu tangu apate taarifa za mwanaye kufariki kule Tanga, hajawahi kukaa sawa maana alibadilika ghafla na kwa kipindi chote alikuwa Hospitali ya KCMC. Alishindwa hata kumzika mwanaye kutokana na mshituko alioupata kufuatia kifo hicho. Kifo chake kimetuumiza sana kama familia, kupoteza watu wawili kwa wakati mmoja ni pigo kubwa," amesema Jerome.
![](https://i.ytimg.com/vi/FuSIB6xq5K4/maxresdefault.jpg)