Baada ya maandamano makubwa yaliyofanyika juzi nchini Kenya na kusababisha vifo vya takribani watu 22 na kusababisha Rais William Ruto kukubali kuuondoa muswada tata wa Sheria ya fedha, vijana wa Gen-Z wameandamana tena jana wakitaka kiongozi huyo ajiuzulu.
Licha ya Rais Ruto kutekeleza matakwa yao ya kuuondoa muswada huo, siku moja kabla, bado vijana hao wameendelea na maandamano yao, huku wakilalamika kwamba kiongozi huyo amewasaliti baada ya kuingia madarakani Agosti 2022.
Katika kampeni zake za uchaguzi, Ruto alijipambanua kama mgombea wa kupinga mfumo uliopo na akaahidi kutekeleza sera za kuweka fedha zaidi kwenye mifuko ya Wakenya. Alikuwa akitumia msemo wa 'hustler' akimaanisha yeye ni mpambanaji na atawainua wapambanaji wengine kama 'kina mama mboga'.
Hata hivyo, wafuasi wake walianza kuvunjika moyo baada ya Serikali yake kuondoa ruzuku muhimu za mafuta na unga wa mahindi. Wakenya wengi waliona hili kama usaliti.
Ruto, mara kwa mara, amekuwa akiwataka Wakenya kufunga mikanda. Hata hivyo, ziara yake rasmi nchini Marekani, Mei mwaka huu, ilizua utata alipokodi ndege ya kifahari badala ya kutumia ndege ya rais au ya Shirika la Ndege la Kenya (Kenya Airways).
Hata hivyo, baadaye, baada ya kelele kuwa nyingi, Ruto alisema kuwa ndege hiyo iliyokodiwa ililipiwa na marafiki ambao hakuwataja.
Kwa mujibu wa Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu inayofadhiliwa na Serikali ya Kenya, idadi ya vifo ilikuwa 22 siku ya Jumatano, na 19 kati ya hao waliripotiwa jijini Nairobi.
Wakati huohuo, Jeshi la Polisi lilisema vifo vilikuwa vimefikia 30 na vilirekodiwa Githurai pekee, ambako ni nje ya Nairobi, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa.
Hali ilivyokuwa jana
Polisi wa Kenya wamewafyatulia risasi za mpira na mabomu ya machozi waandamanaji jijini Nairobi jana, huku wengine wakirejea barabarani, licha ya Rais William Ruto kufuta Muswada wa Sheria ya Fedha uliopendekeza ongezeko la kodi. Maandamano hayo yakiongozwa na idadi kubwa ya vijana, yalizipuuza mamlaka, huku Serikali ya Ruto ikibaki njiapanda namna ya kudhibiti machafuko hayo yasilete madhara kwa raia.
Makumi ya waandamanaji walikusanyika katika eneo la katikati mwa Jiji la Nairobi, huku wanajeshi wakiwa wametumwa na polisi waliovalia zana za kuzuia ghasia wakizuia njia za kuelekea ofisi za Ikulu na bungeni, kwa mujibu wa AFP. Maofisa waliwafyatulia risasi za mpira na mabomu ya machozi kwa makundi madogo ya waandamanaji na kuwakamata takriban watu saba huku vurugu zikizuka na baadhi ya waandamanaji wakiwarushia polisi mawe.
"Vijana hawatapumzika, hatuna imani na Ruto ambaye awali awafananisha waandamanaji na wahalifu,” alisema Lucky Otieno (27), ambaye ni mhitimu wa chuo kikuu wakati akizungumza na Shirika la AFP.
“Ni mustakabali wetu tunaopigania, maslahi ya Wakenya,” alisema.
Mitaa mingi katika jiji la Nairobi maduka mengi yalifungwa, huku wafanyabiashara wakihofia machafuko zaidi.
Pia, makundi ya vijana waliandamana katika mji wa Mombasa na ngome ya upinzani ya Kisumu, huku wengine wakifunga barabara na kuwasha moto katika mji huo.
Baada ya majengo ya bunge kuvamiwa juzi na polisi kuwafyatulia risasi waandamanaji, Ruto alibadilisha msimamo kuhusu ongezeko la kodi, lakini tofauti na ilivyotarajiwa, hali hiyo ilichochea maandamano.
Hata hivyo, waandamanaji walishikilia msimamo wao wa kuandamana jana kuwakumbuka waliouawa katika maandamano hayo.
Mbunge wa Congress ya Marekani, Ilhan Omar alisema matumizi ya nguvu yaliyoonekana wakati wa maandamano yaliyofanyika Kenya yanadhoofisha misingi ya kidemokrasia.
Aliandika kupitia ukurasa wake wa X, Omar pia alisema ni “Lazima waandamanaji wabaki na amani”.
Akijadili suala hilo, mtafiti katika Taasisi ya Masomo ya Usalama (ISS), Willis Okumu amesema Rais Ruto anachelewesha muda.
“Nadhani [Ruto] anachelewesha muda tu," alisema, alipokuwa akizungumza na Al Jazeera kuhusu tangazo la Rais wa Kenya la kuondoa muswada huo.
“Nadhani ameambiwa kuwa hii ina madhara kisiasa. Inawezekana shinikizo kutoka kwa mataifa ya Magharibi limechangia. Alikuwa anahitaji kutuliza hali baada ya kufanya makosa na anajaribu kuwaridhisha vijana. Amegundua atapoteza nchi.
“Siamini kuwa ni ya kweli; mambo hayo yote, sidhani kama atayatekeleza. Amekuwa rais kwa miaka miwili na hajatimiza chochote kati ya alichoahidi.”
Ещё видео!