DC GONDWE ATOA SIKU 3 KWA WAKUU WA IDARA TEMEKE.
Mkuu wa wilaya Temeke Mh.Godwin Gondwe ametoa siku tatu kuanzia leo kwa wakuu wa Idara ya manispaa hiyo kuhakikisha wanakutana na wamiliki wa nyumba zilizomo kwenye eneo la shule ya Sekondari Kingugi wilayani humo.
Ametoa agizo hilo alipokuwa akizungumza na wakuu hao wa idara mara baada ya kukagua eneo la shule hiyo ambalo ndani yake kuna nyumba tatu za wananchi jambo linaloleta usumbufu kwa wanafunzi na wakazi hao.
"Natoa siku tatu kwenu kuhakikisha mnakutana na wamiliki hawa pale ofisini kwa Mkurugenzi kufanya tathimini upya ili waweze kulipwa na kuhama eneo hili".Alisema Mkuu huyo wa wilaya
Mmoja wa wamiliki wa nyumba hizo Bi.Mwashabani Katundu anayedai kuwepo eneo hilo kwa takribani miaka 16 sasa alimueleza mkuu wa wilaya kuwa wapo tayari kuhama eneo hilo muda wowote endapo serikali itawalipa fidia itakayowezesha kujenga eneo lingine.
"Hapa unaponiona nashindwa hata kujenga chochote maana tuliambiwa tusiendeleze kujenga maana tunatakiwa kuhama".Alisema Bi.Mwashabani.
Mwanasheria wa Manispaa hiyo Bw.Salum Papen alishauri suala hilo liangaliwe kwa umakini na kupewa kipaumbele kwa maslahi mapana ya wanafunzi hao ambao wanahitaji kuwa kwenye mazingira tulivu ya kujifunzia.
Shule hiyo ya Kingugi iliyopo kata ya Kiburugwa katika manispaa ya Temeke mkoani Dar es salaam iliyojengwa katikati ya makazi ya wananchi imekuwa ikilalamikiwa na wanafunzi na wadau mbalimbali kuwa mazingira yake sio tulivu kwa elimu.
![](https://i.ytimg.com/vi/QWQBFeTKjSg/mqdefault.jpg)