Polisi wa kutuliza ghasia nchini Kenya walitumia gesi ya kutoa machozi Jumatatu kuwatawanya waandamanaji waliokusanyika mjini Nairobi, na kwingineko nchini, kwa maandamano yaliyoitishwa na kiongozi wa upinzani Raila Odinga na wenzake wa muungano wa kisiasa wa Azimio la Umoja - One Kenya.
Maandamano hayo yaliitishwa kupinga kupanda kwa gharama ya maisha, kumtaka Rais William Ruto na utawala wake kuondoka mamlakani, na kupinga mchakato unaoendelea, wa uteuzi wa makamishna wa tume ya uchaguzi na mpipaka, kati ya mengine.
Vyombo vya habari vimeripoti kwamba angalau watu 22, wakiwemo wabunge, walikamatwa kwa kushiriki maandamano hayo, ambao yaliharamishwa na polisi jana Jumapili.
Waandamanaji pia waliwarushia mawe polisi wa kupambana na ghasia nje ya ofisi za serikali katika mji mkuu.
"Tutakuwa hapa hadi gesi ya kutoa machozi imalizike," mwandamanaji mmoja, Markings Nyamweya, 27, aliliambia shirika la habari la AFP.
![](https://i.ytimg.com/vi/QsjWQejyZ5o/mqdefault.jpg)