Baadhi ya madereva wa bajaji katika Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, wamelalamikia kutozwa Sh500 kila siku, bila kupewa risiti ya malipo halali, huku wakiwa hawajui matumizi ya fedha hizo.
Mwananchi Digital imepita katika njia ya KCMC na kushuhudia vijana wawili wakiwa eneo la Ushirika na wanasimamisha kila bajaji inayopita na kutoza Sh500, huku zile zinazogoma kusimama wakizikimbiza, kisha kuning'inia pembeni.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, madereva hao wamedai fedha hizo wamekuwa wakitozwa kwa nguvu na wanapokataa hukamatwa na bajaji zao kuzuiwa kwa siku nzima.
Wakizungumza wanaokusanya fedha hizo eneo la geti la Ushirika, wamesema fedha hizo ni makubaliano ya madereva bajaji kwa ajili ya kusimamia utaratibu wa bajaji hizo na kiasi wanachokusanya wanajilipa kama posho.
Viongozi wa chama cha bodaboda mbali na kukiri kuwepo kwa tozo hiyo ya Sh500, wamedai ni kwa ajili ya posho ya vijana wanaofanya kazi ya kusimamia bajaji hizo na fedha hizo hazifiki kwenye chama.
Hata hivyo, alipoulizwa kwa nini wanasimama barabarani kukusanya fedha na si kwenye vituo ambako bajaji huanzia, amesema wanapokaa barabarani wanasaidia kudhibiti vitendo vya kihalifu na mvurugano wa bajaji kutoka njia moja kwenda nyingine.
Akizungumzia malalamiko hayo, Ofisa Mfawidhi wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (Latra) Mkoa wa Kilimanjaro, Paul Nyello amesema suala la madereva wa bajaji kutozwa Sh500, haliwahusu na kumtaka mwandishi wa habari awatafute viongozi wa bajaji na bodaboda.
Manispaa ya Moshi, inakadiriwa kuwa na bajaji zaidi ya 3,000, ambazo zinafanya shughuli ya usafirishaji katika maeneo mbalimbali, ikiwemo KCMC, Majengo, Rau, Soweto,Pasua, Bonite, Kahe na Mabogini.
![](https://i.ytimg.com/vi/c3-9URnTtec/maxresdefault.jpg)