Watu wanne wa familia moja, akiwemo mama wa bwana harusi, wamefariki dunia kwa ajali ya gari wakitokea harusini jijini Dar es Salaam kuelekea Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro.
Ajali hiyo imetokea usiku wa kuamkia Jumatatu Juni 24, 2024 katika eneo la Bwiko, Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga baada ya gari walilokuwa wakisafiria, aina ya Toyota Noah, kuacha njia na kupinduka na kusababisha vifo na majeruhi kadhaa waliokuwemo ndani ya gari hilo.
Alipotafutwa kwa njia ya simu, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi kuzungumzia ajali hiyo, amesema yupo kwenye kikao atafutwe baadaye.
“Nipo kwenye kikao, naomba unitafute baadaye,” amesema Kamanda Mchunguzi.
Hata hivyo, ndugu wa marehemu hao, Fredrick Michael amesema wanafamilia hao walifariki kwa ajali njiani wakati wakitoka Dar es Salaam kwenye harusi ya ndugu yao ambayo ilifanyika Jumamosi Juni 22, 2024.
Amewaja waliofariki katika ajali hiyo kuwa ni mama mzazi wa bwana harusi, Cecilia Luka na dada yake, Antonio Luka pamoja na ndugu wawili wa bwana harusi ambao ni Godfrey Michael na Judith Michael.
Diwani wa Kata ya Kirongo Samanga, wilayani Rombo, Prisila Shayo amesema wamepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za vifo vya wanafamilia hao kwa kuwa ndugu hao waliondoka kwa pamoja kwenda kwenye sherehe ya harusi ya ndugu yao.
Soma zaidi katika tovuti ya Mwananchi
(Imeandikwa na Frola Temba na Janeth Joseph)
Ещё видео!